TANGAZA NASI

header ads

Covid-19:DC akanusha hakuna tishio la Corona “walikuwa ni wasafiri wa kawaida”



Njombe/Wanging'ombe

Mkuu wa wilaya ya Wanging’ombe mkoani Njombe,Ally Kasinge amesema serikali imejiridhisha kutokuwepo kwa tishio lolote la Corona wilayani Wanging’ombe isipokuwa watanzania waliokuwa wakitoka  jijini Dar es Salaam  siku ya jana kuja mkoani Njombe kwa kutumia usafiri wa basi la kampuni la Luwidzo walikuwa ni wasafiri wa kawaida.

Kasinge ametoa ufafanuzi wakati wa mahojiano na mmoja wa waandishi wa habari wa kituo cha radio cha ICE FM Makambako ili kuwatoa hofu wakazi wa mji wa Makambako,wilaya ya Wanging’ombe na mkoa wa Njombe kwa ujumla,kutokana na taarifa zilizokuwa zikisambaa mitandaoni pamoja na maeneo hayo juu ya kushikiliwa kwa basi la kampuni ya Luwidzo kutokana na kushtukiwa kuwa mgojwa ambaye ni muathirika wa maradhi yanayotokana na Corona alitumia usafiri huo.

“Ukweli ulivyo baada ya kufuatilia kupitia vyombo vya dola sisi wilaya ya Wanging’ombe tukishirikiana na wenzetu wa Njombe kwa maana ya OCD wa Makambako tulifanikiwa kuipata gari ambayo ilisadikika kuchukua abaria hao,na abiria wenyewe tuliwapata,tukapata nafasi ya kuwahoji na kufuatili huko walikotoka tumetumia watendaji wa serikali,wataalamu wa sekta ya afya kujua historia ya mtaa walikotoka,wilaya walikotoka na tumejiridhisha kwamba hakuna tishio lolote la Corona isipokuwa hao walikuwa ni wasafiri wa kawaida kama walivyokuwa wasafiri wengine”alisema Ally Kasinge

Awali mkuu huyo wa wilaya amesema serikali ilipata taarifa kutoka kwa rai kuwepo kwa mwananchi ambaye familia yake inaishi jijini Dar es Salaam na kutokana na tatizo la Corona imelazimika familia yake (watoto) wake awahamishe kwa muda na kuwaleta Wanging’ombe mkoani Njombe ambako yeye anaishi na familia nyingine.

“Kwa maana hiyo tukalazimika kupitia jeshi la polisi na vyombo vingine vya usalama kufuatilia taarifa hizo na tukajirisha kweli wapo vijana wanao kuja Wanging’ombe kwa misingi hiyo ya hofu iliyopo katika jiji la Dar es Salaam”alisema Kasinge

Aidha amesema taarifa walizokuwa wamezipata awali kwa raia ni kuwa vijana hao walikuwa wanaishi jirani na nyumba ambayo kumekuwa na mgonjwa anayesadikika kuwa ni muathirika wa virusi vya Corona ndio maana wakalazimika kufanya uchunguzi.Huku akibainisha kuwa kitu kilichounganisha matukio hayo kwa sasa ni kutokana na janga hilo kuchukua nafasi kubwa Dar es Salaam hivyo upo uwezekano wa watu kurudi mikoani kutokana matukio hayo hivyo imekuwa ni rahisi wananchi kudhani kila anayetoka jijini Dar es Salaam anaweza kuwa muathirika au pengine amekuwa akishirikiana kwa karibu na waathirika wa ugonjwa huo.

Hata hivyo mganga mkuu wa halmashauri ya mji wa Makambako Dkt,Alexandra Mchome,amesema ni kweli walishtukiwa watu watatu wa familia moja hivyo amewatoa hofu wananchi wa Makambako kutokana taaratibu za kushtua zilizofanywa jana na watu hao walio dhaniwa hawakuwa na maambukizi.

“Tulichokifanya ni kujiridhisha kama nikweli watu hao wanamaambukizi ya Corona? Na tukajihakikishia kwamba wale watu walikuwa ni salama na tuliwapumzisha shule ya Makambako na asubuhi wameruhusiwa waendelee na safari,hivyo hakuna mtu yeyote ambaye yuko karantina mpaka sasa na basi la Luwidzo lilibeba watu ambao wako salama”alisema Mchome

Hata hivyo hapo jana kupitia mtandao wetu wa blog na kurasa za mitandao ya kijamii tulichapisha taarifa hii ya kuthibitishwa kuwepo kwa mgonjwa anayetokana na virusi vya Corona (Covid-19) kuwa ametoroka karantini jijini Dar es salaam,huku  mkuu wa wilaya ya Njombe Ruth Msafiri akithibitisha kushikiliwa basi za kampuni ya Luwinzo mjini Makambako zilizotumiwa na mgojwa huyo na ukaguzi ukiendelea.kutokana vyanzo vyetu vya habari

Taarifa ilisema mkuu wa wilaya ya Njombe Ruth Msafiri amesema serikali inafuatilia  kwa karibu chombo cha usafiri kilichotumiwa na mgonjwa aliyetoroka karantini jijini Dar es salaam.Na kunukuliwa

“Hizo taarifa ni za kweli lakini bado wanafanyia kazi hawajanipa taarifa ni Luwinzo ipi kwasababu zipo Luwinzo tatu,kwa hiyo wameisha kamata Luwinzo ya Kwanza wanasubiri zingine na zote baadaye watakagua watathibitisha ni ipi na itabaki hiyo hiyo moja”alisema Ruth Msafiri

Aidha mkuu huyo wa wilaya ameto wito kwa wananchi kuendelea kujikinga na virusi hivyo vya Corona.

“Wito wangu ni kwamba lazima tukubali Corona ipo na dawa ya kwanza unikinge,nikukinge yaani tukingane na inapotokea umethibitika utulie na utapata huduma zote sasa unapokimbia unaleta taharuki  na unaleta shida kwasababu unaleta ugonjwa kutoka eneo moja kwenda eneo linguine”amesema Ruth Msafiri

Vile vile alisema serikali haitaruhusu watu kukusanyika wala kukimbilia katika maeneo yaliyowekwa kwa ajli ya washtukiwa na badala yake wananchi waache vyombo vya tiba na vya usalama kusimamia swala hilo.

Kutokana na mkanganyiko wa taarifa hizo,Njombe Press blog inaomba radhi kwa wasomaji wetu walioweza kupatwa na taharuki.

Tanzania bado ina visa vipya 53 vya ugonjwa wa corona hatua inayoongeza idadi ya watu walioathirika na ugonjwa huo kufikia watu 147.Kutokana na taarifa iliotumwa kwa vyombo vya habari,waziri wa Afya Ummy Mwalimu siku kadhaa zilizopita ,Ummy alisema kwamba wagonjwa wote ni raia wa Tanzania.
Idadi hiyo ni kubwa zaidi kutangazwa kwa siku moja katika taifa la Tanzania tangu wagonjwa wa kwanza wa virusi hivyo kugunduliwa katika eneo hili.

Ummy alisema miongoni mwa wagonjwa hao 38 wanatoka katika mkoa wa Dar es salaam, 10 katika Kisiwa cha Zanzibar , mmoja kutoka Kilimanjaro , 1 kutoka Mwanza , Pwani Mtu 1 na Kagera mtu 1.



Post a Comment

0 Comments