TANGAZA NASI

header ads

Tanzania:Tiketi za usafiri kuanza kukatwa kwa njia ya mtandao


SERIKALI imesema mfumo wa kukata tiketi kwa njia ya mtandao, utaanza hivi karibuni kwa mabasi yote ya mikoani,lengo likiwa ni kupunguza msongamano vituoni ikiwa ni sehemu ya kuendelea kukabiliana na corona.

Waziri wa ujenzi, uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwele, wakati wa ukaguzi wa mifumo Dar es Salaam jana, alisema utaanza kufanya kazi karibuni na kiu ya Serikali ni kuona wananchi wananufaika kwa kuondoshewa adha ya usafiri.

Alisema Serikali imefikia hatua ya mwisho ya kutumika mfumo huo ambapo wananchi watatumia simu kukata tiketi.

“Mfumo huu utasimamiwa na Serikali kupitia kituo chetu cha Data center, utasaidia wananchi wetu hususani wale wa chini ambao walikuwa wanaingia gharama kwenda katika vituoni kukata tiketi.

“Tumefika wakati wa kuwa kisasa zaidi, wapiga debe walikuwa wakiongeza gharama lakini wakati huu wa maambukizi ya corona ni muhimu kutafuta njia mbadala katika usafirishaji.

“Hakuna sababu ya msafiri kutembea na pesa mkononi, hata wanaopandia njiani ni wakati wa kuwa na pesa kwenye simu, kwakuwa hatuna uhakika iwapo ugonjwa huu utaenea hadi kwenye noti, ni lazima kuwa na njia nyingi za udhibiti,”alisema Kamwele

Alisema wamiliki wa mabasi walikuwa na maswali mengi wakati wa mchakato wa mfumo huo, wakihofia kupata hasara lakini yeye anaamini utanufaisha pande zote.

 “Mtu akikata tiketi Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Mamlaka ya Udhibiti wa usafiri Ardhini (LATRA) na wenye mabasi kila mmoja atapata mgao wake mara tiketi inapokatwa,”alisema.

Aliitaka Data Centre kuhakikisha mifumo hiyo inadhibitiwa katika gharama za uendeshaji kwakuwa lengo lake ni kupunguza gharama za usafiri kwa mwananchi.

Meneja wa Data centre, Geofrey Mpangala, alisema  kwa kushirikiana na wakala mtandao, mapema wiki hii maelekezo yote ya Serikali kuhusu mradi huo yanakamilika ili kukamilisha huduma.

Chanzo:Mtanzania digital


Post a Comment

0 Comments