TANGAZA NASI

header ads

Prof.Ole Gabriel awataka watalaam wa mifugo kuacha kukaa ofisini

 
Na.Mwaandishi wetu,Chato
 
Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo) Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka wataalam wa sekta ya mifugo kote nchini watumie muda mwingi kwenda kuwahudumia wafugaji badala ya kukaa ofisini.

Prof. Ole Gabriel ameyasema hayo mara baada ya kufika kukagua moja ya kliniki za mifugo iliyopo Wilaya ya Chato Mkoani Geita leo ambapo amemshauri Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo Bw. Leonard Mwaisabula kutenga kiasi cha fedha cha kuanza ukarabati wa kliniki hiyo na Wizara yake itamuunga mkono kwa kukamilisha hatua zilizobaki.

"Ni kweli Wizara ina mpango wa kukarabati kliniki zote za Mifugo hapa nchini lakini kipaumbele chetu cha kwanza ni kwa zile halmashauri ambazo zitakuwa zimeshaanza ukarabati kwa kutumia fedha za mapato yao ya ndani hivyo kama Chato mkianza mapema Wizara pia itawapa kipaumbele na hatimaye muwe mfano kwa wengine",Aliongeza Prof. Ole Gabriel.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato Bw. Leonard Mwaisabula amesema kuwa halmashauri yake itayafanyia kazi ushauri huo kwa sababu wana shauku kubwa ya kuona kliniki hiyo inafanya kazi.

"Nimepokea ushauri wako Mhe. Katibu Mkuu na kesho tutakutana kwa ajili ya kuangalia mchanganuo wa fedha tulizokuwa tumetenga kwenye idara ya mifugo ili kuona namna tunavyoweza kuanza na ukarabati wa kliniki hii kwa sababu kwetu ina umuhimu Mkubwa sana" Alisema Bw. Mwaisabula.

Mara baada ya kutoka kwenye eneo hilo Prof. Olr Gabriel alielekea kwenye eneo la mnada wa Buzirayombo unapotarajiwa kujengwa mnada mkubwa wa upili ambako alioneshwa kuridhishwa na usanifu wa michoro inayoonesha namna mnada huo utakavyokuwa baada ya kukamilika kwake.

"Lakini pia nimeona eneo hili la mnada litakuwa linajumuisha pande mbili zinazotenganishwa na barabara hivyo Mkurugenzi kwa kushirikiana na Wakala wa Majengo (TBA) ni lazima muangalie namna ya kufanya ili kuhakikisha wananchi wanakuwa salama wakati wote wakiwa kwenye eneo la mnada" Aliongeza Prof. Ole Gabriel.

Pia alipendekeza kutokana na michoro ya mnada huo kuonesha ni wa kisasa ni lazima kuwe na mfumo mzuri wa matangazo ndani ya eneo la mnada, kituo kizuri cha Polisi kitakachofanya kazi kwa saa 24, Mfumo wa kibenki na huduma za afya zitakazowanufaisha wananchi wote watakaokuwa karibu na eneo hilo la mnada, Runinga kubwa itakayoonesha kila kinachoendelea Mnadani hapo na mfumo mzuri wa kuhifadhi idadi na aina ya bidhaa na huduma zinazopatikana mnadani hapo ili kuwe na utaratibu wa kupata taarifa zote muhimu ndani ya muda mfupi.

Kwa upande wake Meneja wa TBA Mkoa wa Geita Mhandisi Gladys Jeffa aliishukuru Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa ushirikiano Mkubwa iliowaonesha mpaka sasa ambapo aliahidi kufanya kazi nzuri itakayokamilika kwa wakati.

"Tunataka kuhakikisha mpaka kufika mwisho wa Mwezi Mei tuwe tumekamilisha na kuwasilisha hii hatua ya michoro yote ya mnada huu na tunataka kabla ya kuvuka mwaka huu wa fedha mkandarasi awe site" Alisisitiza Mhandisi Jeffa.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato Bw. Leonard Mwaisabula alisema mradi huo kwao una manufaa makubwa kwa sababu utaongeza kiasi cha makusanyo ya fedha za ndani na hivyo kuiwezesha Halmashauri kuboresha miundombinu ya huduma mbalimbali za jamii kama vile Elimu na afya.
 
credit:Fullshangweblog

Post a Comment

0 Comments