TANGAZA NASI

header ads

Madereva wa vyombo vya moto waonywa kushiriki kwenye matendo maovu kuelekea kwenye uchaguzi



Na Amiri Kilagalila,Njombe

Serikali mkoani Njombe imetoa onyo kwa madereva wa boda boda, bajaji, daladala na taksi kuepuka kutumika vibaya  na watu wenye malengo maovu hasa kipindiki hiki kuelekea uchaguzi mkuu wa madiwani,wabunge na Rais.

Kauli hiyo imetolewa na mkuu wa wilaya ya Njombe Ruth Msafiri akimuwakilisha mkuu wa mkoa wa Njombe mhandisi Marwa Rubirya kwenye semina iliyoandaliwa ili kuyajengea uwezo makundi hayo yaweze kufanya kazi kisasa pamoja na kuwaunganisha na fursa za kiuchumi

 Amesema wapo watu wanaodhani kipindi cha uchaguzi ndiyo hasa cha kufanya vurugu hivyo aliwataka kupuuza mawazo hayo na kutofanyia kazi ushauri wa namna hiyo.

Vile vile amesema katika kipindi hiki kuelekea uchaguzi umakini utakuwa wa hali ya juu kwani watu wa aina tofauti wataongezeka mkoani hapa tofauti na ilivyokuwa awali ambao wana tabia tofauti hivyo aliwataka wenyeji kukataa kutumika vibaya.

"Sisi wenyeji tuhakikishe kwamba Njombe tuliyonayo tunataka baada ya uchaguzi ibaki kama ilivyokuwa awali tukiwa na viongozi wapya watakaoenda kututumikia" Alisema Ruth Msafiri.

Aidha amesema makundi hayo yote ni wafanyakazi hivyo wanapokodishwa waendelee kufanya shughuli zao kwani wana vyombo vya usafiri ukizingatia kuwa kipindi hiki ni cha fursa hivyo wazitumie vizuri.

Aidha alizitaka taasisi za fedha kuendelea kushirikiana na serikali na kukaa kwenye vikao vyao ili kuona umuhimu wa kuhudumia vikundi hivyo kwa mtazamo tofauti na ule ukopaji mwingine kwa kuangalia muda wa kudai marejesho pamoja na riba.

 "Vile vile muangalie mikopo ya kuwalea kwa kuanza na mikopo midogo ya kati na atakayemudu katika mikopo mikubwa" Alisema Ruth Msafiri.

 Nae muandaaji na muwezeshaji katika  semina hiyo Sady Mwang'onda alisema lengo kubwa la semina hiyo ni kuwajengea uwezo makundi hayo kwa kutoa elimu kwa kundi hilo amblo limeonekana kuachwa kupewa elimu hasa katika namna bora ya kufanya kazi zao kisasa.

 Alisema vijana wengi wanaojiajiri kwenye bodaboda, bajaji na taksi wengi wao wametoka mtaani na hawajapata mafunzo yeyote kisha wanaingia barabarani hivyo kuna vitu vingi wanapaswa kuvifahamu ili kufanya kazi zao kwa weledi.

"Nchi yetu ina vijana wengi wa namna hivyo kwa kupata elimu hii itawasaidia kuanzia sasa na kuendelea kwa kufanya biashara zao kwa ufanisi" Alisema Mwang'onda.

Mratibu wa mafunzo ya usalama barabarani mkoa wa Njombe Koplo Marwa Kisyeli aliwataka waendesha vyombo vya moto kuzingatia elimu ambayo imekuwa ikitolewa mara kwa mara na jeshi la polisi kaika kukabiliana na ajali za barabarani.

"Tumesema utaenda mwendo kikomo maana yake ni mwendo ambao hutakiwi kuvuka lakini wapo madereva taksi anaendesha gari spidi mia na bajaji pia chombo cha matairi matatu kinatembea zaidi ya spidi sitini ikitokea ajali hapo ni kifo hivyo tutawaliwe na elimu" Alisema Marwa.

 Nao washiriki wa semina hiyo ambao ni madereva bodaboda, bajaji, daladala na taksi akiwemo Alberto Myamba na Yuda Mlowe walisema wameshukuru kupata mafunzo hayo kwani yamewasaidia kufahamu namna nzuri ya kufanya kazi zao kisasa kujiepusha watu wenye nia mbaya katika kipindi hiki kuelekea uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na raisi.

"Boda boda wameonekana wakishiriki katika vitendo viovu lakini kupitia semina tuliyoipata tutabadilika na kufanya kazi zetu kwa uaminifu mkubwa" Alisema Alberto Myamba.

"Nimejifunza kama dereva unapokuwa unamiliki gari ni vizuri kukata bima kubwa ili hata chombo kikipata shida yeyote unaweza kulipwa" Alisema Yda Mlowe.

Mafunzo hayo yalishirikisha  madereva bodaboda, bajaji, dala dala, taksi, wadau wa taasisi za fedha, bima ya afya, bima za mali pamoja na jeshi la polisi.

Post a Comment

0 Comments