TANGAZA NASI

header ads

Mkurugenzi wa Biharamulo aagizwa kusimamia ukusanyaji wa Mapato



Na. Angela Msimbira KAGERA

Halmashauri ya Wilaya ya Biharamuro Mkoani Kagera  imeendelea kususua katika suala la ukusanyaji wa mapato na kusababisha maendeleo ya Halmashauri hiyo kuzorota kutokana na baadhi ya viongozi kushindwa  kusimamia suala hilo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo wakati akiongea na uongozi wa Mkoa wa Kagera  kwenye ziara  ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Halmashauri ya Manispaa ya  Bukoba, Mkoani Kagera.

Mhe. Jafo amesema  hali ya ukusanyaji wa mapato katika Mkoa wa Kagera ni nzuri isipokuwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Biharamuro ambayo  hali ya ukusanyaji imekuwa  ikisusua na kupelekea Halmashauri hiyo kushindwa kutekeleza miradi ya maendeleo kwa wakati.

 “Halmashauri zinategemea makusanyo ya mapato kwa ajili ya kujiendesha, hivyo zikishindwa kukusanya mapato zinapelekea kushindwa kutimiza malengo waliojipangia kwa mwaka na kushindwa kutoa huduma bora kwa jamii.” Amesisitiza Mhe. Jafo

Anafafanua kuwa hali ya ukusanyaji wa mapato katika Halmashauri hiyo hairidhishi kutokana na baadhi ya watumishi wasiokuwa waaminifu  kucheza na ukusanyaji wa mapato, hivyo kuisababishia halmashauri kuwa nyuma kimaendeleo.

Amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Biharamuro kuhakikisha anasimamia suala la ukusanyaji wa mapato na kutoa adhabu kali kwa watumishi ambao hawafuati sheria, taratibu na miongozo kweye suala la ukusanyaji wa Mapato

Mhe. Jafo amewaagiza viongozi wote nchini waliopewa dhamana kuacha kufanyakazi kwa mazoea bali watumie taaluma zao katika kuwahudumia wananchi maskini wenye uhitaji katika jamii

Akikagua ujenzi wa Miundombinu ya barabara Mkoa wa Kagera Mhe. Jafo amesema ameridhishwa na ujenzi wa barabara hizo zilizojengwa chini ya mradi wa uimarishaji Miji (ULGSP) jambo ambalo limebadilisha sura na muonekano wa Mji huo.

Aidha Mhe. Jafo yupo kwenye ziara ya Kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo inayosimamiwa na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa katika Mikoa ya Rukwa, Mpanda, Kigoma, Kagera na Geita

Post a Comment

0 Comments