Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo ameridhishwa na kasi ya ujenzi unaoendelea katika Hospitali ya Wilaya inayojengwa katika Mji wa Katoro, Mkoani Geita.
Waziri Jafo ameyasema hayo wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo ya ujenzi wa Hospitali hiyo iliyoanzwa ilianza kujegwa mwezi 2, 2020 na inategemewa kukamilika ifikapo mwezi juni, 2020.
Amesema kuwa fedha za ujenzi wa Hospitali hiyo zilitolewa na Serikali mwezi Februari lakini hadi kufikia sasa kazi imekamilika kwa asilimi 90 tofauti na Halmashauri nyingine ambazo ziliingiziwa Fedha mapema.
“Nimeridhika na kasi ya ujenzi unaoendelea katika Hospitali ya Katoro na hasa nimefurahishwa na utekelezwaji wa maagizo yangu niliyoyatoa ya kuongeza nguvu kazi, sasa naona kazi imeweza kufanyika ndani ya miezi minne tofauti na baadhi ya Halmashauri nyingine. Hili ni jambo la kujivunia kwa Halmashauri ya Mji wa Geita” ameeleza Waziri Jafo.
Waziri Jafo ameutaka uongozi wa Mkoa wa Geita kuhakikisha wanasimamia ujenzi wa Hospitali hiyo ili kuweza kukamilika kwa wakati uliopangwa.
Aidha, Hospitali ya Katoro ni moja kati ya Hospitali za Halmashauri za Wilaya 67 zilizojengwa na Serikali kwa ajili ya kusogeza huduma za afya karibu na wananchi.
Wakati huohuo, Waziri Jafo amekagua Mradi wa Ujenzi wa Stendi ya Kisasa ya mabasi, Uwanja wa Mpira wa Miguu na upanuzi wa Hospitali ya Wilaya ya Chato ambapo ameridhishwa na ujenzi wake na amesisitiza ukamilishaji wa haraka utakaozingatia ubora wa miradi hiyo.
0 Comments