TANGAZA NASI

header ads

Ufaransa kukarabati jengo la Uwanja wa Ndege

 


Ufaransa imeonesha nia ya kuisaidia Tanzania katika ukarabati wa jengo la pili la abiria katika Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, ambao ulijengwa kwa mkopo kutoka Serikali ya Ufaransa pamoja na kushirikiana katika kukuza biashara na uwekezaji pamoja na masuala ya ulinzi na usalama.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Profesa Palamagamba Kabudi, alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Ulaya na Mambo ya Nje wa Ufaransa Jean Yves Le Drian, jijini Paris, ambapo katika mazungumzo hayo Ufaransa imekubali kushirikiana na Tanzania katika masuala ya maendeleo, uwekezaji na biashara.

Aidha Profesa Kabudi, ameongeza kuwa Ufaransa imepokea ombi la Tanzania la kupatiwa Euro milioni 718 kama msaada ama mkopo kwa ajili ya kusaidia katika maeneo mbalimbali ya maendeleo ikiwemo awamu ya tano ya ujenzi wa mradi wa mabasi ya mwendo kasi Jijini Dar es Salaam,Ujenzi wa Uwanja wa Ndege Mwanza na miradi ya nishati ya jua na maji.

Kwa upande wake Waziri wa Ulaya na Mambo ya Nje wa Ufaransa, Jean Yves Le Drian, amemhakikishia Profesa Kabudi kuwa Ufaransa itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo inayofadhiliwa na serikali ya Ufaransa kupitia shirika lake la maendeleo la AFD pamoja na kuwashawishi wawekezaji na wafanyabiashara wa Ufaransa  kuwekeza Nchini Tanzania kwenye sekta mbalimbali.

Post a Comment

0 Comments